Advertisements

Wednesday, February 22, 2017

Dk. Kigwangalla afunguka Maandhimisho ya Miaka 25 ya Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala, ameungana na Wadau wa Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC) katika kuadhimisha miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Tume hiyo. Akizungumza katika ufunguzi, Dkt. Kigwangala amesema kuwa katika kipindi cha miaka 25, Tume hii imekuwa mstari wa mbele katika kushirikiana na Serikali na Wadau wengine katika kuhakikisha huduma za Jamii zinatolewa kwa kuzingatia ubora na uwiano mzuri.
Rais wa Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC), Askofu Dkt. Alex Malasusa, akizungumza na Wajumbe na wageni mbalimbali waliohudhuria katika kumbukumbu ya miaka 25 tangu kuanzishwa kwa Tume hiyo. Kumbukumbu hizo zinafanyika tarehe 21/02/2017 katika Ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam. 

“Kulingana na taarifa nilizopewa, kwa sasa Tume ina taasisi za elimu zaidi ya 1000. Hizi zinajumuisha shule na vituo vya kutolea Elimu ya awali, shule za Elimu ya Msingi na Sekondari, Vyuo vya ualimu, vituo vya mafunzo ya ufundi stadi na Vyuo vya Elimu ya Juu. Kwa upande wa Sekta ya Afya, nimeambiwa mna vituo vya afya vipatavyo 900. Hii ni pamoja na hospitali 102, vituo vya afya 102 na zahanati zipatazo 696. "Vilevile kuna takribani taasisi zipatazo 58 za kutolea mafunzo ya wataalamu wa Afya na pia kuna Vyuo Vikuu. Ni dhahiri kabisa, taasisi zote hizi zinatoa mchango mkubwa katika nchi yetu na pia zimeiwezesha jamii yetu kupata huduma za elimu na afya zilizo bora,” alisema Dkt. Kigwangala.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala, akitoa hotuba ya ufunguzi katika maadhimisho ya miaka 25 ya Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC), yanayofanyika tarehe 21/02/2017 katika ukumbi wa Diamond Jubilee , jijini Dar es Salaam.

Maadhimisho hayo yanapambwa kwa kauli mbiu isemayo “Wito wa Kuelimisha na Kuponya Jamii: Changamoto na Mafanikio ya utoaji wa huduma za jamii Tanzania”, yamehudhuriwa na Mh. Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu Tanzania, Waheshimiwa Maaskofu, akiwemo Rais wa Tume hiyo Askofu Dkt. Alex Gehaz Malasusa, Makamu wa Rais wake, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu, Mganga Mkuu wa Serikali, pamoja na Wadau mbalimbali wa Tume hiyo. Katika hatua nyingine, Naibu Waziri Kigwangala, pia alitoa rai kwa Wadau wa Tume hiyo hususan kwa Taasisi zote za Afya zilizo chini ya CSSC, kuwa na uwazi na uwajibikaji katika matumizi ya rasilimali fedha ili kuhakikisha kuwa hudum a za afya zinamfikia kila mlengwa. Na pia aliongeza kwamba uendeshwaji wa vituo hivi vya afya uende sambamba na sera ya afya ya nchi.
Baadhi ya Washiriki wanaohudhuria katika maadhimisho ya miaka 25 ya Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC), wakimsikiliza ,Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala wakati akitoa hotuba ya ufunguzi . Maadhimisho hayo yanafanyika tarehe 21/02/2017 katika ukumbi wa Diamond Jubilee , jijini Dar es Salaam.

Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC) ni chombo kilichoundwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT) mwaka 1992 kwa dhumuni la kuratibu na kusimamia huduma za kijamii zitolewazo na Taasisi za Makanisa husika za Elimu na Afya nchini.
Baadhi ya Maaskofu waliohudhuria katika maadhimisho ya miaka 25 ya Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC) wakimsikiliza Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala (Hayupo pichani). Kutoka kulia ni Askofu Severine Niwemugizi ( Jimbo Katoliki la Rulenge), Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Mwanza, Judah Thadei Rwaichi, akifuatiwa na Askofu Telesphor Mkude wa Jimbo Katoliki la Mororogoro.
Makamu wa Rais wa Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa (Jimbo la Iringa), akimpongeza Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala mara baada ya kutoa hotuba fupi ya ufunguzi katika maadhimisho ya miaka 25 ya Tume hiyo. Kutoka kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa CSSC, Bw. Peter Maduki, na kulia kwake ni Rais wa Tume hiyo, Askofu Dkt. Alex Malasusa.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala wa pili kutoka kushoto akiwa pamoja na Rais wa Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC), Askofu Dkt. Alex Malasusa (katikati), pamoja na Makamu wa Rais wa Tume hiyo, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa (kushoto). Wengine ni Mganga Mkuu wa Serikali, Prof Mohamed Bakari na kulia kwake ni Mkurugenzi Mtendaji wa CSSC, Bw. Peter Maduki. Hii ni katika maadhimisho ya miaka 25 ya kuanzishwa, Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii, yanayofanyika tarehe 21/02/2017 katika ukumbi wa Diamond Jubilee, Dar es Salaam.

No comments: