Advertisements

Monday, July 17, 2017

Familia yapata mtoto wa kike baada ya miaka 137!

Will Settle na mkewe, Kelen wakiwa na mtoto wao, Carter
NI mtoto wa kike! Ndivyo kila mmoja katika familia ya Settle alivyohamaki, mara baada ya kuzaliwa kwa binti yao, Carter Loiuse Settle Juni 25, mwaka huu.

Kuzaliwa kwa Carter, binti wa Kelen (36) na mumewe, Will Settle (38) kumeonekana kuwa sawa na baraka katika ukoo wa baba wa mtoto. Ni baraka kwa kuwa, kwa miaka 137 hakuwahi kuzaliwa mtoto wa kike katika ukoo wa Settle, wenye maskani yao katika Jimbo la South Carolina, Marekani.

“Hakika tulijua atazaliwa mtoto wa kike,” anasema na kuendelea; “Lakini kilichoendelea kilimwacha kila mmoja akipagawa kwa furaha na kutoamini kilichotokea.” Anasema wazazi wa Will ndio waliokuwa na furaha zaidi.

Ndiye aliyefichua kwamba, kwa miaka 137 hakuwahi kuzaliwa mtoto wa kike katika familia yao. “Atakuwa malaika katika familia. Ameleta furaha kubwa ndani ya nyumba,” anasema Kelen, mama wa mtoto huyo.

Carter hatakosa ndugu wa kiume maishani, kuanza mababu, wajomba, mabinamu, na hata kaka yake mwenye umri wa miaka 7, Rowland aliyepatikana katika ndoa ya awali ya Will. “Rowland anampenda sana mdogo wake, habanduki pembeni yake,” anasema Kelen akiwa mwenye tabasamu wakati wote.

Si Rowland na Kelen tu ambao wamefurahishwa na ujio wa mtoto huyo, bali familia nzima ambayo inapishana kutwa, kucha kumwangalia mtoto huyo sambamba na kumwagia zawadi. Majirani, marafiki na watu wengine pia wamekuwa wakiitembelea familia hiyo mara kwa mara kwa lengo la kujionea miujiza baada ya miaka 137.

Kelen na mumewe wanasema kwa kuwa hawakutarajia kupata mtoto wa kike, walichagua jina la Carter, hivyo hata alipozaliwa waliendelea na uamuzi wake, kwamba aitwe Carter. Will anasema hata kazini kwake kulikuwa na chereko kutokana na kuzaliwa kwa mtoto wa kike baada ya zaidi ya karne moja kwenye ukoo wao.

“Will anafanya kazi katika kampuni ya matangazo ya mabango, kwa hiyo wenzake walipoona katika mtandao wa Facebook walitengeneza bango kubwa. Ilikuwa kitu cha kushitukiza na kupendeza kwetu, bonge la zawadi,” anasema Kelen ambaye ni mzungumzaji zaidi kuliko mumewe.

Imeshatokea kwa mtoto Carter, je atazaliwa mtoto mwingine wa kike katika familia hiyo au ni jambo la kusubiri karne nyingine? Ni mipango ya Mungu, hata hivyo ni jambo la kusubiri na kuona

HABARI LEO

No comments: